Somo la 1: Kutoka Kusoma Hadi Kuelewa
Somo hili limetafsiriwa kutoka katika Copr. 2017, Bruce N. Cameron, J.D. Marejeo yote ya maandiko yametoka kwenye tafsiri ya New International Version (NIV), copr. 1973, 1978, 1984 International Bible Society, isipokuwa kama itaelezwa vinginevyo. Nukuu kutoka kwenye tafsiri ya Biblia ya NIV inatumika kwa ruhusa ya Wachapishaji wa Biblia wa Zondervan. Majibu yaliyopendekezwa yanapatikana kwenye parandesi (kwenye mabano). Somo limekaa kimtazamo kwamba mwalimu anatumia ubao au sehemu nyingine yoyote ambayo inaweza kuonekana na wanafunzi. Kama huwa una kawaida ya kupokea somo hili kwa njia ya barua pepe na hukulipata kwa juma moja, unaweza kulipata kwa kubofya kwenye www.lesoni.blogspot.com kwa lugha ya Kiswahili na http://www.GoBible.org kwa lugha ya Kiingereza pamoja na lugha nyingine kama vile Kifaransa, Kijerumani. Omba kwa ajili ya uongozi wa Roho Mtakatifu unapojifunza.
Utangulizi:Kwa sasa ninasoma kitabu kizuri sana kinachoelezea kwa nini wapinzani wakubwa wa Mungu ni mazuzu/wapumbavu. Kauli hii inaweza kuonekana kuwa si ya kistaarabu, lakini kitabu hiki kimejaa ucheshi na mantiki, na kinatoboa tundu kwenye kile kinachoitwa upuuzi wa kisayansi unaoshambulia uwepo wa Mungu hadharani. Tatizo langu ni kwamba ninaposoma baadhi ya hoja zenye mantiki kwenye kitabu, ninatafakari juu ya hoja hizo ili kuhakikisha kuwa ninaelewa kile ninachokisoma. Huo ndio unaopaswa kuwa uchunguzi wetu kila mara. Hata pale tunaposoma jambo tunalodhani kuwa tunalielewa, tunatakiwa kujipatia nafasi ya muda ili kuwa na uhakika. Kisha tunatakiwa kuchimbua kama kile tulichokielewa kinaleta mantiki. Hilo ndilo somo letu juma hili. Tunapoanza kuchimbua kitabu cha Danieli, je, kweli tumejiandaa kukielewa? Je, utofauti fulani-fulani unaleta mantiki? Hebu tuzame kwenye Biblia na tuone kile tunachoweza kujifunza!
- Hekima ya Mungu
-
- Soma 1 Wakorintho 1:18. Hii inaashiria tahadhari gani kuhusu kueneza injili kwa wasioamini? (Tusichukulie kwamba wataelewa. Wanaweza kudhani kwamba tunazungumza upuuzi.)
-
-
- Hata kama wanaelewa maneno yetu, je, watauelewa ujumbe wetu?
-
-
-
- Ikiwa umejibu, hapana, tunawezaje kueneza injili?
-
-
- Soma 1 Wakorintho 1:19 na Isaya 29:14. Mungu anatumia njia gani kwenye hekima ya kipagani? (Ataiangamiza na kuikatisha tamaa. Nadhani kitabu ninachokisoma kimantiki kinaangamiza hekima ya kipagani.)
-
-
- 1 Wakorintho 1:19 inarejelea Isaya 29:14 inaposema “imeandikwa.” Isaya anapendekeza kuwa hekima ya ulimwengu itapoteaje? (“Ajabu na mwujiza” vitaangamiza hekima ya kiulimwengu.)
-
-
-
-
- Unadhani hiyo inamaanisha nini? (Uvumbuzi wa kisayansi wa hivi karibuni kwamba ulimwengu unatanuka, hivyo kimantiki ni kwamba ulimwengu una mwanzo, uliishia kwenye nadharia ya “Uibukaji” (Big Bang). Kabla ya hapo, imani ya kisayansi ilikuwa ni kwamba ulimwengu ulikuwa tuli (static), na hivyo hakuna nguvu kutoka nje iliyohusik)
-
-
-
-
-
- Tafakari kidogo nadharia ya “Uibukaji.” Inahitaji nini? (Inahitaji nguvu kutoka nje. Inahitaji nguvu nyingi ili kujionyesha. Haya “maajabu” husababisha matatizo mengi kwa wanasayansi wanaopinga dhana ya mungu wa nje.)
-
-
-
- Soma 1 Wakorintho 1:20-21. Je, hii inaashiria kwamba Mungu hataki wenye hekima wa duniani wamjue yeye? Kwamba hatuwezi kueneza injili? (Soma 1 Wakorintho 1:27. Sidhani kama Paulo anajenga hoja kwamba hatuwezi kueneza injili au kwamba Mungu anawakataa watu walioelimika sana. Badala yake, anajenga hoja kwamba Mungu anatenda kazi kupitia udhaifu wa mwanadamu. Tafakari jinsi Yesu alivyokuja duniani na jinsi alivyokufa. Hekima ya kidunia inakataa jambo hili. Kama Mungu aliwakataa watu werevu na wenye elimu, asingemchagua Paulo kwa kuwa alikuwa mtu mwenye elimu kubwa sana.)
-
- Soma Danieli 2:31-36. Tutajifunza kwamba Mungu aliwaacha watu wote wa Babeli wenye hekima na kufunua maana ya ndoto kupitia kwa Danieli, mateka wa Kiyahudi. Unafahamu nini kuhusu tafsiri ya ndoto hii? (Inaweka wazi mustakabali wa ulimwengu! Hii inaonesha kwamba Mungu anatenda kazi kupitia kwenye udhaifu.)
-
-
- “Udhaifu” unamaanisha nini katika muktadha huu? Je, Danieli alikuwa dhaifu? Je, alikuwa mkimya? Hakuwa na elimu? (Hapa udhaifu unamaanisha kwamba hakuwa sehemu ya mfumo wa nguvu ya kipagani.)
-
-
- Unajifunza nini kuhusu njia ya uelewa wa Mungu kutokana na kile tulichokijadili? (Kitu bora ambacho ulimwengu wa kipagani unaweza kukitoa si rahisi kikakuelekeza kwenye tafsiri sahihi ya mapenzi ya Mungu.)
- Unabii
-
- Hivi karibuni nimesoma kwamba kuna tofauti kati ya unabii wa “zamani” na unabii wa “ufunuo.” Baadhi ya wasomi wanatangaza aina mbalimbali za nadharia hii. Ninachotaka tukitafakari ni madai mahsusi kwamba unabii wa zamani unaweza kuishia kutokuwa wa kweli kwa sababu unategemea “majibu ya kibinadamu.” Unabii wa ufunuo, kwa upande mwingine, mara zote utakuwa wa kweli. Je, hii inamaanisha kwamba hatuwezi kuamini unabii wote?
-
-
- Je, ukweli wa unabii unaendana na jinsi tunavyouona?
-
-
-
- Una maoni gani kuhusu madai haya?
-
-
-
- Unadhani tofauti hii inatusaidia kuelewa vizuri zaidi kile tunachokisoma kwenye Biblia?
-
-
- Hebu tuangalie mfano. Soma Zekaria 9:1-4. Huu unapewa jina la unabii wa “ufunuo.” Lakini, hebu ruka vifungu kadhaa hadi Zekaria 9:9-10. Huu ni unabii kuhusu ujio wa Yesu na hivyo kudhaniwa kwamba ni unabii wa “zamani” kwa maana ya kwamba hautegemeani na jibu la kibinadamu. Je, unaweza kuelezea tofauti kati ya unabii huu wa aina mbili? Je, unabii unabadilika kutoka unabii wa aina moja hadi unabii wa aina nyingine katika sura moja?
-
- Soma Zekaria 14:1-4. Hii ni sehemu ya unabii wa “zamani” kuhusu mustakabali wa Yerusalemu, ikimaanisha kwamba inaweza isiwe kweli kutegemeana na jibu la kibinadamu. Una maoni gani kuhusiana na jambo hili? (Licha ya kuelewa matamanio ya wasomi kuainisha vitu, nadhani madai kuhusu kuaminika kwake ni tatizo. Angalao mtetezi mmoja wa tofauti hii anaitumia kuondosha matarajio kwamba matukio ya mwisho ya historia yatajitokeza katika Mashariki ya Kati. Kwa kuwa matukio ya mwisho bado hayajatokea, kupuuza uwezekano huu kunaiweka hekima ya kibinadamu (kuupa unabii majina sahihi) juu ya neno la Mungu.)
-
-
- Kuna sababu gani kuamini kwamba unabii wa Zekaria 14:1-4 ni wa kuaminika kidogo kuliko unabii wa Zekaria 9:9-10?
-
-
- Soma Yona 1:2, Yona 3:4, Yona 3:10 na Yona 4:1-2. Je, Yona alidhani kwamba huu ulikuwa unabii wenye masharti? (Ndiyo na hapana. Ana hasira kwa sababu anadhani kwamba unabii haukuwa na masharti. Lakini, anatambua kwamba Mungu ni “mwenye neema na huruma.”)
-
-
- Je, Mungu alidhamiria unabii huu kuwa na masharti (wa zamani/wa watu)? (Angalia tena Yona 3:10. “Mungu akaghairi.” Hii inamaanisha Mungu alibadili mawazo yake. Haimaanishi kwamba alidhamiria kuacha matokeo yabadilike kwa jinsi watu walivyoitikia.)
-
-
-
- Ukikataa kuupa majina unabii mapema tofauti na uhalisia wake, utapendekeza nadharia gani badala yake? (Fikiria jambo hili: Mungu wetu ni wa neema, ana huruma, hana hasira, mwenye upendo, na tabia yake inaendana na mawazo yake kuhusu kupeleka janga. Hii inawafanya wafuasi wake watumaini tu kwamba Mungu atatenda jambo sahihi. Ninapendelea njia hiyo.)
-
- Mpangilio wa Muda (Timing)
-
- Hapo awali tulisoma ndoto ya Mfalme Nebukadreza. Hebu tusome tafsiri katika Danieli 2:37-41 na Danieli 2:44-45. Wasomi wanatofautiana kama hii ni ishara tu, jambo lililotokea siku za nyuma, jambo litakalotokea siku zijazo, au jambo linaloelezea mzunguko wa historia ya dunia. Unalionaje hili?
-
-
- Kuna hoja gani dhidi ya hii kuwa ishara ya mawazo ya jumla? (Soma Danieli 2:37-38. Danieli anasema unabii una matumizi mahsusi.)
-
-
-
- Hoja ni ipi dhidi ya unabii kuelezea tu matukio ambayo bado hayajatokea? (Soma Danieli 2:39. Danieli hasemi tu kwamba matukio yanatukia sasa hivi, bali pia anasema kuwa ndoto inaelezea mfululizo wa falme zitakazoibuka na kuanguka katika siku zijazo – na sasa tunaweza kuona hili limeshatokea.)
-
-
-
- Hoja ni ipi dhidi ya ndoto kuelezea matukio ya nyuma pekee? (Soma tena Danieli 2:44-45. Utabiri wa Ufalme wa Mungu usio na mwisho unaoangamiza falme nyingine zote bado haujatokea.)
-
-
- Unadhani kwa nini Mungu alimpa Mfalme Nebukadreza hii ndoto? Kwa nini aitoe ndoto hii katika kipindi hiki katika historia? (Yerusalemu iliangamizwa. Watu wa Mungu walichukuliwa mateka na taifa lililokuwa na uhasama na Mungu wa kweli. Mfuasi wa Mungu anaweza kuwa na wasiwasi wenye mantiki kwamba Mungu hakuwa na udhibiti. Ndoto hii pamoja na tafsiri yake ilionesha kwamba Mungu ana historia yote ya ulimwengu iliyopangiliwa.)
-
- Tutajifunza ndoto hii kwa undani zaidi, lakini je, inazungumzia nini kuhusu uwepo wa Mungu wetu? (Kwanza, inaniambia kuwa Mungu ni halisi. Kamwe Nebukadreza asingeweza kuota kwa usahihi falme ambazo zingeufuatia ufalme wake. Kamwe Danieli asingeweza kuyasoma mawazo ya Nebukadreza. Ukweli kwamba ndoto hii tayari imeshatimia inatupatia ujasiri kwa Mungu anayejishughulisha na mambo ya wanadamu na aliyeanzisha Ufalme wake wa milele.)
-
- Rafiki, kwa nini usimtumaini Mungu kwa ajili ya mustakabali wako? Je, utajitoa kufanya hivyo leo?
- Juma lijalo: Kutoka Yerusalemu Hadi Babeli.